Jumatatu, 14 Februari 2022

KAMATI YA SOKO KUJENGA SKULI TUMBE PEMBA

 



NA ZUHURA JUMA, PEMBA

KAMATI ya soko la samaki na mboga mboga Tumbe Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba, imesema imedhamiria kujenga skuli ya maandalizi na msingi, ili kuwapunguzia watoto masafa marefu ya kuifuata huduma hiyo.

Kamati hiyo imesema kuwa, walikaa pamoja na kutafakari kitu cha kufanya katika kuisaidia Serikali kufikisha huduma za kijamii kwa wananchi, ambapo walipendekeza kujenga skuli.

Walisema kuwa, watoto wa shehia mbili za Tumbe huifuata huduma hiyo masafa marefu, hivyo wameona ni vyema angalau kuwapunguzia masafa hayo wanafunzi wa maandalizi na msingi kutokana na kuwa wao ni wadogo.

Walieleza kuwa, wamekuwa wakikusanya fedha kutoka kwa wavuvi wanaotumia bandari ya Tumbe na kuziingiza katika akaunti yao ya soko, hivyo wameona kiasi cha fedha walichonacho ni vyema wakaisaidia Serikali katika kuwafikishia wananchi huduma za kijamii.

Katibu wa Kamati ya Soko hilo Rashid Khatib Hamad alisema, kwa sasa kwenye akaunti yao kuna zaidi ya shilingi milioni 19 ambazo wamezikusanya tangu mwaka 2016.

“Kamati hii ilianzishwa na wavuvi wenyewe na wameiridhia, hivyo fedha tunazokusanya hapa kila siku, inapofika mwisho wa mwezi asilimia 20 inakwenda halmashauri ya Wilaya yetu na asilimia 80 inapelekwa kwenye akaunti ya soko na ndio hiyo ambayo tunataka tujenge skuli”, alisema mwenyekiti huyo.

Alieleza kuwa, wameshaona eneo la kujenga skuli hiyo ingawa mmiliki wa eneo hilo anahitaji apatiwe angalau eneo jengine litakalomsaidia kufanya shughuli zake za kumpatia kipato ikiwa ni pamoja na kilimo.

“Kwa kushirikiana na Jumuiya yetu ya Maendeleo ya Tumbe, tupo kwenye harakati za kumtafutia eneo jengine mwananchi huyo japo la Serikali, ili tupate kuanza ujenzi huo wa skuli”, alisema Katibu huyo.

Alisema, makusanyo yote yanayopatikani yanatokana na mnada, ambapo wanayaweka kwa ajili ya matumizi ya soko, kuisaidia jamii pamoja na kuipatia Serikali mapato yake, ambapo kila mvuvi anatakiwa kutoa asilimia tatu ya mauzo yake kwa siku.

Aidha alisema kuwa, hivi karibuni walikwenda kufungua akauti katika benki ya CRDB kwa ajili ya kuwawezesha na kuwaboresha wavuvi kwa kuwatafutia mashine na boti za kisasa ambazo zitawawezesha kufika mbali na kuvua samaki wakubwa.





Aliwataka wavuvi hao waelewe kwamba kinachofanyika baada ya makusanyo hayo ni suala la maendeleo kwa jamii, hivyo wawe wepesi katika kuchangia kwa ajili ya soko na jamii ya Tumbe kwa ujumla.

Kwa upande wake Katibu wa Kamati ya wavuvi Tumbe Omar Hamad Salim alisema yeye anahusika na kukusanya fedha kwa kila boti ambazo zinatia nanga katika bandari ya Tumbe.

“Fedha hizi zinatusaidia pale ambapo wavuvi wamepatwa na dharura, hivyo tunaweka mafuta kwenye boti na kwenda kuwaokoa na pia tunachangia kwenye huduma za kijamii kwa kushirikiana na kamati yetu ya soko”, alisema Katibu huyo.

Alieleza, hivi karibuni kuna kiwanja kimeuzwa kwa ajili ya kujengwa hospitali ya Tumbe, hivyo walitakiwa wapeleke laki saba, ambapo tayari wameshazitoa sambamba na kusaidia mipira ya maji kwa ajili ya kufikisha huduma hiyo msikitini.

Kwa upande wao wavuvi Hamad Suleiman Mwinyi na Horera Suleiman Zahran wamesema ni jambo zuri ambalo wanataka kulifanya, kwani itakuwa wamechangia kuimarisha huduma za kijamii katika shehia zao.

Mwananchi Khadija Suleyum mkaazi wa Tumbe alisema kuwa, iwapo watajenga skuli hiyo watakuwa wameisaidia sana jamii, kwani watoto wadogo wanakwenda skuli masafa marefu.

Nae Ali Hassan Sheha alieleza kuwa kamati hiyo ikiwa itajenga skuli, wananchi wataelewa kwamba mapato yanayopatikana kwa wavuvi hayaliwi na mtu mmoja bali ni kwa manufaa ya wanajamii wote wa Tumbe.

                                                       MWISHO.

SIKU YA REDIO DUNIANI, NAIBU WAZIRI AWAPA NENO WAANDISHI W AHABARI TANZANIA

 


NA HAJI NASSOR

Naibu Waziri wa Habari na Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mh Andrew Kundo amewataka waandishi wa habari nchini kuboresha maudhui wanayoyarusha katika redio mbalimbali nchini ili kuongeza uaminifu kwa wasikilizaji kwa kurusha taarifa zilizochunguzwa kwa kina na kujenga jamii yenye maisha bora.


Akizungumza mapema hii leo wakati wa maadhimisho ya siku ya Redio duniani yaliyoandaliwa na Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma katika ukumbi wa Maktaba Mpya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na UNESCO akimwakilisha Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mh. Nape Nauye, Naibu Waziri amesema uaminifu kwenye uandishi wa habari za redio unategemeana na maidhui ya hali ya juu yanayotengenezwa.

"Ukuaji huu wa redio umesaidia sana kufikisha taarifa kwa urahisi kwa wananchi, tafiti mbalimbali zinaonesha vituo hivi vya redio maarufu kama redio za mikoani au redio za jamii zinasikikizwa zaidi kwenye maeneo zilizopo kutokana na ukweli kwamba zinarusha maudhui yanayogusa wananchi wa maeneo hayo, hivyo waandishi lazima waendelee kujikita kwenye taarifa ambazo zinafanyiwa uchunguzi na ambazo zitakuwa na manufaa kwa umma na zitasaidia kujenga jamii yenye maisha bora baadae" amesema.

Amesema, kutokana na maendeleo ya kidijitali kumekuwa na wimbi kubwa la kutoheshimu maadili ya uandishi wa habari kutokana na usambazaji wa taarifa zinazokosa weledi, hivyo amevitaka vituo vya habari viwe sehemu ya maisha ya wasikilizaji wao kwa kuzalisha maudhui yanayoendana na hadhira wao ili kuendeleza imani kwa wasikizaji.

Vilevile katika hotuba yake ya uzinduzi wa maadhimisho ya siku ya redio duniani, Naibu Waziri wa Habari na Mawasiliano Mh Andrew Kundo, amevihakikishia vituo vya habari nchini kuvitatulia changamoto zinazovikumba kwa kushindwa kuendana na teknolojia ya sasa kufuatia viwango vya kati vya biashara, hivyo kuangalia namna ya kuviwezesha kujitegemea kifedha na kujiamini na kubaki kwenye biashara hasa katika kipindi hiki kigumu cha Uviko-19, kutokana habari, mawasiliano na TEHAMA kuwa fursa katika redio na kupelekea kuimarisha utoaji huduma zao.

Kwa upande wake Mratibu wa maadhimisho hayo Abdallah Katunzi, ameeleza kuwa siku ya redio duniani ina umuhimu mkubwa wa kukuza uelewa na umuhimu wa redio kwa jamii, kuhamasisha viongozi na watunga sera kufikisha taarifa kwa jamii na kutengeneza mshikamano kati ya taasisi za Habari ndani ya jamii husika.

Mwakilishi Mkazi wa UNESCO nchini Tanzania Bwn. Tirso Dos Santos amesema redio inabaki kuwa chombo muhimu sana katika maendeleo ya jamii kutokana na mchango mkubwa wa kuhabarisha jamii juu ya masuala mbalimbali ya uwajibikaji wa viongozi, mapambano dhidi ya Uviko-19, harakati za kumuinua mwanamke na kuwapa kipaumbele watu wa makundi maalumu kujiinua kiuchumi kutokana na mijadala mbalimbali inayowekea na vyombo vya habari nchini.

Maadhimisho ya siku ya redio duniani yanafanyika kila mwaka tarehe 13 Mwezi wa 2, ambapo kwa mwaka huu maadhimisho haya yanafanyika kwa mara ya 11 yenye kauli mbiu "Redio na Uaminifu".

Alhamisi, 10 Februari 2022

NAIBU BALOZI WA IRELAND AIPA TANO PACSO

 



 

NA HAJI NASSOR, PEMBA

NAIBU Balozi wa Ireland nchini Tanzania Mags Gaynor, ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa umiliki wa rasilimali ardhi kwa wanawake, uliokuwa ukitekelezwa na Mwemvuli wa asasi za kirais Pemba ‘PACSO’ na kumalizika hivi karibuni.

Naibu Balozi huyo alisema, kutokana na majibu ya wanufaika wa mradi huo alivyozungumza nao, ameridhishwa na utekelezaji wa mradi huo, na hasa kwa kuwafikia walengwa.

Alisema mradi huo ulilenga kuwafikia wanawake ili kuwajengea uwelewa, juu ya umilikiwa wa rasilimali ikiwemo ardhi, jambo ambalo sasa, limewanufaisha hasa kwa kuwepo wanufaika waliopata haki zao.

Naibu Balozi huyo aliyasema hayo ofisi za PACSO Chake chake Pemba, kwenye kikao cha tathimi kilichojumuisha wanufaika wa mradi wa uongozi wa PACSO.

Alieleza kuwa, kwa vile wapo wanawake kisiwani Pemba walionufaika moja kwa moja, ikiwa ni pamoja na kurithi, kununua ardhi na kulalamikia ucheleweshaji urithi ni hatua kubwa.

“Serikali ya Ireland, imeridhishwa mno na mradi huu uliokuwa ukiendeshwa na ‘PACSO’ na tutangalia uwezekano wa kuendeleza kuhusiasna na elimu kwa jamii,’’alieleza.

Katika hatua nyingine, Naibu huyo Balozi wa Ireland Mags Gaynor, alisisitiza haja kwa wanufaika hao kuwafikishia wenzao elimu ya umuhimu wa umiliki rasilimali.

Alisema kuwapa mradi huo PACSO rasilimali fedha hazikupotea, kutokana na kuwanufaisha walengwa, waliokuwasudiwa ndani ya jamii husika.

Mmoja wa wanufaika hao Fatma Khamis Juma wa Wawi, alisema awali hakuwa akiona umuhimu wa umiliki wa rasilimali, ingawa baada ya mafunzo, sasa ameamka.

“Hata urithi sasa tumesharithi, maana niliwaambia kaka zangu kuwa sasa turithi, na tumesharithi baada ya kuwaelimisha ingawa walikuwa wazito,’’alieleza.

Mratibu wa miradi kutoka PACSO, Mohamed Najim Omar, alisema licha ya mradi huo kuwa wa miezi miwili, lakini umefikia lengo lao.

“Pamoja na kwamba mradi ulikuwa wa miezi mwili, lakini wanawake kwa asilimia 60 na wanaume asilimia 40, walifikiwa na kunufaika kwa kupata elimu,’’alieleza.

Nae Salama Mtondoo kutoka Wete, alisema licha ya kuwa na kesi yake mahakamani ya kutapeliwa na kiongozi wa serikali ardhi yake, lakini mafunzo hayo yamempa hamasa zaidi.

“Mafunzo ya umiliki wa ardhi, na hasa siku ile ya kuzitambua sheria za ardhi, kwangu yamenipa uwelewa zaidi, wa kuendelea na kesi yangu,’’alieleza.

Sheha wa shehia Vitongoji wilaya ya Chake chake, Ayoub Suleiman, alisema katika kipindi cha mwezi Januari hadi Febuari alipokea malalamiko 40 ya wanawake juu ya ardhi.

“Baada ya kupata mafunzo ya umiliki wa rasilimali hasa ardhi, sasa hata malalamiko katika shehia yangu yameongezeka kutoka 25 ya mwaka 2021, hadi kufikia 40 kwa kipindi cha miezi mwili kwa mwaka huu,”alisema.

Afisa Mipango wilaya ya Chake chake Kassim Ali Omar, alisema wamepokea maombi 20 kwa mwaka huu, ya wanawake wakiomba kununua na kuuza ardhi zao.

Katibu mkuu wa ‘PACSO’ Sifuni Ali Haji, alisema mradi huo wanatarajia unawezaa mwengine kutokana na mafanikio makubwa waliyoyapata.

Katika utekelezaji wa mradi huo, awali kulifanyika uzinduzi wa mradi, kongamano, mafunzo ya siku nne ya umiliki ardhi pamoja na kuzifahamu sheria za usimamizi ardhi.

                                          Mwisho  

 

 

 

Attachments area